Habari motomoto zilizojili hivi punde kutoka kila kona ya Dunia

Wednesday, 28 December 2016

KOREA YASAIDIA SH MILIONI 105 KWA AJILI YA WAATHIRIKA WA TETEMEKO LA ARDHI MKOANI KAGERA


SERIKALI ya Jamhuri ya Korea imetoa msaada wa Dola za Marekani 50,000 (Sh milioni 105) za kwa ajili ya waathirika wa tetemeko la ardhi lililotokea mkoani Kagera Septemba 10, mwaka huu.

Msaada huo ulikabidhiwa Dar es Salaam jana na Balozi wa Korea nchini, Song Geum Young na kupokewa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dk Augustine Mahiga kwa niaba ya Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.
Baada ya kupokea msaada huo, Dk Mahiga aliishukuru Serikali ya Korea na kuahidi msaada huo ataukabidhi kwa Waziri Mkuu ili uweze kutumika kama ulivyokusudiwa. Alisema Korea imekuwa mbia mkubwa wa Tanzania tangu nchi hiyo ilipoanzisha uhusiano wa kidiplomasia na Tanzania miaka 25 iliyopita.
Alieleza katika kipindi hicho Tanzania imekuwa ikipokea misaada mbalimbali ya kiuchumi, kijamii na ya kibinadamu ukiwemo msaada huo wa fedha uliolekezwa kwa waathirika wa tetemeko la ardhi la mkoani Kagera.
Waziri huyo alitaja misaada ambayo Korea imeipatia Tanzania kuwa ni pamoja na ujenzi wa daraja la Malagarasi mkoani Kigoma, ujenzi wa hospitali ya kisasa ya Mloganzila wilayani Kinondoni, Dar es Salaam na ujenzi wa hospitali ya uchunguzi wa afya ya Mama iliyopo Chanika, Ilala, Dar es Salaam.
Naye Balozi wa Korea nchini aliahidi kuwa nchi yake itaendelea kushirikiana na Tanzania hususan kutoa misaada ya maendeleo ili iweze kutimiza azma ya Serikali ya awamu ya tano ya kuifanya Tanzania kuwa nchi ya viwanda.

No comments:

Post a Comment