Habari motomoto zilizojili hivi punde kutoka kila kona ya Dunia

Wednesday, 28 December 2016

VIJIJI VYOTE NCHINI KUPATA UMEME NDANI YA MIAKA 10 IJAYO




SERIKALI imesema vijiji vyote ambavyo havijafikishiwa huduma ya umeme vitapata huduma hiyo kupitia mradi mkubwa wa umeme vijijini Awamu ya Tatu unaotekelezwa na Wakala wa Umeme Vijijini (REA), unaotarajiwa kuanza hivi karibuni.

Hayo yalisemwa hivi karibuni na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo katika ziara yake mkoani Mara ya kukagua utekelezaji wa mradi wa umeme vijijini awamu ya pili (REA II) ambao unamalizika.
Katika maeneo mbalimbali aliyotembelea Muhongo, alielezwa kuwa vijiji vya ndani havina umeme kwani nishati hiyo imeishia kwenye vijiji vilivyopo katika barabara kubwa na kwenye vituo vya biashara.
Alisema serikali inatambua vijiji ambavyo havikufikishiwa huduma hiyo, hivyo aliwaasa wananchi katika vijiji hivyo kuwa na subira kwani lengo la serikali ni kuhakikisha ndani ya miaka 10 vijiji vyote nchini viwe vimefikiwa na umeme.
Alisema mradi wa REA III umetengewa zaidi ya Sh trilioni moja ambayo ni mara tatu zaidi ya iliyotengwa katika mradi wa REA II ambao unamalizika kwa kuunganisha baadhi ya vijiji.
Aliongeza kuwa sasa serikali ipo katika utaratibu wa kuwapata wakandarasi mahiri ambao watakabidhiwa jukumu la kutekeleza mradi huo ambao ni mkubwa.
Akizungumzia mradi huo wa REA III, Meneja wa Kanda ya Ziwa wa Shirika la Umeme (Tanesco), Amos Maganga, alisema mbali na kuunganisha vijiji vyote, pia mradi huo umelenga kuhakikisha unamaliza mapungufu yaliyojitokeza katika REA II.
Alisema katika utekelezaji wa mradi wa REA II kuna mapungufu yaliyojitokeza kwa sababu mbalimbali ikiwemo kutokuwa na wigo mpana, hivyo kusababisha baadhi ya vijiji kurukwa, vingine kutofikiwa na vilevile uhaba wa baadhi ya vifaa katika maeneo mbalimbali.

No comments:

Post a Comment