Habari motomoto zilizojili hivi punde kutoka kila kona ya Dunia

Sunday, 29 January 2017

Simba azama topeni




SIMBA jana ilijiweka kwenye wakati mgumu wa kuendelea kuongoza msimamo wa Ligi Kuu ya Vodacom Bara baada ya kukubali kipigo cha bao 1-0 kutoka kwa Azam.

Katika mechi hiyo iliyochezwa kwenye uwanja wa taifa Dar es Salaam, Simba ilihitaji ushindi au sare kuendelea kujinafasi kileleni mwa msimamo huo lakini sasa matokeo hayo yanaifanya kutoa nafasi kwa mtani wake wa jadi Yanga kuongoza.
Mabingwa watetezi wa ligi hiyo Yanga leo watakuwa uwanjani hapo kucheza na Mwadui na inapewa nafasi kubwa ya kushinda kutokana na ubora wa kikosi chake kulinganisha na wapinzani wao Mwadui ambao katika mechi ya raundi ya kwanza iliwafunga mabao 2-0 mjini Shinyanga.
Yanga ikishinda leo itafikisha pointi 46 na hivyo kuongoza ligi kwa tofauti ya pointi moja dhidi ya Simba yenye pointi 45.
Muuaji wa Simba jana alikuwa John Bocco aliyefunga bao hilo katika dakika ya 70 kwa kuuwahi mpira uliokuwa ukimilikiwa na Method Mwanjali kabla ya kuachia shuti lililotikisa nyavu za kipa Mghana wa Simba Daniel Agyey.
Hii ni mara ya pili kipa huyo kufungwa na Azam tangu alipojiunga na Simba kwenye usajili wa dirisha dogo, kipigo cha kwanza ilikuwa kwenye fainali za kombe la Mapinduzi ambapo Simba pia ililala kwa bao 1-0 lililofungwa na Himid Mao. Mechi hiyo ilipooza karibu kipindi chote cha kwanza ambapo kila upande ulionekana kucheza kwa tahadhari kubwa.
Kipindi cha pili Azam walionekana kuchangamka zaidi na hasa baada ya kupata bao hilo, ambapo Simba nao walianza kufanya mashambulizi ya hapa na pale bila mafanikio.
Simba: Daniel Agyei, Janvier Bokungu/Ibrahim Ajib, Mohammed Hussein, Abdi Banda, Method Mwanjali, Jonas Mkude, Said Ndemla, Jamal Mnyate/Shiza Kichuya, Muzamil Yassin, Pastory Athanas na Juma Luizio/Laudit Mavugo.
Azam FC: Aishi Manula, Erasto Nyoni, Gardiel Michael, Yakubu Mohammed, Aggrey Morris, Stephan Kingue/Mudathir Yahya, Himid Mao, Joseph Mahundi, Frank Domayo, John Bocco/Abdallah Kher na Ramadhani Singano/ Yahya Mohammed.

No comments:

Post a Comment